Katika hitimisho la hotuba yake, Sheikh Dkt. Alhad ametoa wito kwa Masheikh, wazazi, walimu wa dini na viongozi wa jamii kuipa nafasi kubwa Elimu ya Kitwariqa katika mchakato wa malezi ya vijana. “Tukizitumia vizuri Njia hizi za Kisufi katika kuwajenga vijana, tutapata vijana wema, wasikivu, wenye elimu ya dini yao, wenye hofu ya Mungu, na wasio tayari kutumika kuharibu jamii,” amesema.

Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) -ABNA- Tanzania: Sheikh Dkt. Alhad Mussa Salum, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT-TAIFA), ametoa wito mzito kwa Waislamu kuimarisha malezi ya vijana kupitia Njia (Turuq) za Kisufi, akisisitiza kuwa Elimu ya Akhera ndiyo msingi bora wa malezi ya kibinadamu na kijamii.
Akizungumza katika mnasaba wa Maulid ya Mtume Muhammad (saww), Sheikh Dkt. Alhad ameeleza kuwa tarbiyya (malezi) yanayokusudiwa katika Uislamu ni yale yanayomjenga mtu kimwili, kiakili na kiroho, huku msingi wake ukiwa ni Akhera. “Malezi tunayoyakusudia ni Malezi ya Kiislamu. Malezi yanapomlenga mtu kwa upande wa Akhera yake, huo ndio bora zaidi wa elimu. Na malezi bora haya hupatikana ndani ya Njia za Kisufi,” amesema.

Maana Halisi ya Njia (Turuq) za Kisufi
Sheikh Dkt. Alhad amefafanua kuwa Njia au Turuq za Kisufi siyo imani zilizobuniwa bila msingi, bali ni mifumo ya malezi inayojengwa juu ya Qur’an Tukufu na Sunna za Mtume (saww).
Amesema kuwa: “Tunapozungumzia Njia za Kisufi, tunazungumzia maadili, adabu, ucha Mungu, kila kheri na kila jema. Haya yote hupatikana katika Turuq Sufiyyah, na misingi yake kwa undani inatokana na Qur’an na Sunna.”
Kwa mujibu wake, Muislamu anayeishi kwa kufuata misingi ya Njia za Kisufi hujengeka kuwa raia mwema, mcha Mungu, mwenye heshima, nidhamu na uzalendo wa kweli.

Njia za Kisufi na Ulinzi wa Vijana wa Taifa
Sheikh Dkt. Alhad ameeleza kuwa jamii ya leo inakabiliwa na changamoto kubwa ya mmomonyoko wa maadili, hasa kwa vijana, hali ambayo imechangiwa kwa kiasi kikubwa na kuachwa kwa malezi ya kina ya kiroho. “Leo hii tuna upungufu mkubwa upande wa malezi, na tumefeli zaidi kwa vijana. Maadui wamefaulu kumharibu kijana na hata mwanamke, nao wakimharibu, maana yake wameiharibu dunia nzima kimaadili,” amesema.

Amesisitiza kuwa kijana aliyepitia malezi ya Kitwariqa hawezi kuwa miongoni mwa vijana wanaotumiwa vibaya au kuingia kwenye vurugu na maandamano yasiyo na dira, kwa kuwa tayari anakuwa na:
- 1-Utii kwa viongozi wake wa dini
- 2-Nidhamu ya hali ya juu
- 3-Maamuzi yenye busara
- 4-Hofu ya Mwenyezi Mungu
“Huwezi kumkuta kijana wa Kitwariqa akawa katika vijana wa Gen Z wanaotumika kwa kuchochewa. Ni kwa sababu Kijana huyo tayari ana tarbiyya (Malezi bora ya Kiislamu) na muongozo wa kimaadili,” aliongeza nukta hiyo Dkt.Alhad Mussa Salum.

Wito kwa Masheikh na Jamii kwa Ujumla
Katika hitimisho la hotuba yake, Sheikh Dkt. Alhad ametoa wito kwa Masheikh, wazazi, walimu wa dini na viongozi wa jamii kuipa nafasi kubwa Elimu ya Kitwariqa katika mchakato wa malezi ya vijana. “Tukizitumia vizuri Njia hizi za Kisufi katika kuwajenga vijana, tutapata vijana wema, wasikuvu, wenye elimu ya dini yao, wenye hofu ya Mungu, na wasio tayari kutumika kuharibu jamii,” amesema.

Amehitimisha kwa kusisitiza kuwa Uislamu wa kweli ni Uislamu wa maadili, utiifu, amani na kujenga jamii, si Uislamu wa ghasia, vurugu na misimamo ya kihisia.

Your Comment